ALIYEKUWA MTENDAJI WA KIJIJI CHA RUVU REMITI AMEFIKISHWA MAHAKAMANI KWA MAKOSA YA RUSHWA.
NA MWANDISHI WETU MANYARA
Katika Mahakama ya Wilaya ya Simanjiro limefunguliwa shauri la Uhujumu Uchumi *namba 22415/2025* mbele ya Mh. Onesmo Nicodemo Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya wilaya ya Simanjiro dhidi ya aliyekuwa mtendaji wa Kijiji cha Ruvu Remiti Wilaya ya Simanjiro Bw, Godbless Felix Mollel
Mshtakiwa anashtakiwa kwa makosa ya ufujaji na ubadhirifu Kinyume na kifungu cha 28(1) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa sura ya 329 R. E 2022, kikosomwa pamoja na aya ya 21 jedwali la kwanza kifungu cha 57(1) na 60(2) vya sheria ya uhujumu uchumi na pamoja ya kupanga Sura ya 200 R:E 2022.
Aidha mshtakiwa anashtakiwa kwa kosa la wizi akiwa mtumishi wa umma kinyume na vifungu 258 na 270 vya Kanuni za adhabu (sura ya 16 R.E 2022).
Akisoma hati ya mashtaka Mwendesha mashtaka wa TAKUKURU Bw. Faustin Mushi amesema mshtakiwa wakati akitekeleza majukumu yake ya afisa Mtendaji wa Kijiji cha Ruvu Remit alifanyia ubadhirifu fedha za Kijiji kiasi cha Tzs 3,300,000/=, fedha zilizokuwa chini yake kutokana na nafasi yake.
Mshtakiwa amekana kutenda makosa yote yanayomkabili na shauri limehairishwa hadi 25/09/2025 kwa ajili ya kusikilizwa hoja za awali (PH)
Kwa sasa mtuhumiwa yupo nje kwa dhamana baada ya kutimiza masharti ya dhamana ya kuwa na wadhamini wawili ambao wote wamesaini bondi ya Tsh 2,000,000/= kila mmoja.

Comments
Post a Comment